| Chapter 16 |
1 |
"Nimewaambieni hayo kusudi msiiache imani yenu. |
2 |
Watu watawatenga ninyi na masunagogi yao. Tena, wakati unakuja ambapo kila atakayewaua ninyi atadhani anamhudumia Mungu. |
3 |
Watawatendeeni mambo hayo kwa sababu hawamjui Baba, wala hawanijui mimi. |
4 |
Basi, nimewaambieni mambo haya ili saa yake itakapofika mkumbuke kwamba niliwaambieni. "Sikuwaambieni mambo haya tangu mwanzo kwa sababu nilikuwa pamoja nanyi. |
5 |
Lakini sasa namwendea yule aliyenituma; na hakuna hata mmoja wenu anayeniuliza: `Unakwenda wapi?` |
6 |
Kwa kuwa nimewaambieni mambo hayo mmejaa huzuni mioyoni mwenu. |
7 |
Lakini, nawaambieni ukweli: afadhali kwenu mimi niende zangu, maana nisipokwenda Msaidizi hatakuja kwenu. Lakini nikienda, basi, nitamtuma kwenu. |
8 |
Naye atakapokuja atawathibitishia walimwengu kwamba wamekosea kuhusu dhambi, uadilifu na hukumu ya Mungu. |
9 |
Wamekosea kuhusu dhambi kwa sababu hawaniamini; |
10 |
kuhusu uadilifu, kwa sababu naenda zangu kwa Baba, nanyi hamtaniona tena; |
11 |
kuhusu hukumu kwa sababu mkuu wa ulimwengu huu amekwisha hukumiwa. |
12 |
"Ninayo bado mengi ya kuwaambieni, ila kwa sasa hamwezi kuyastahimili. |
13 |
Lakini atakapokuja huyo Roho wa kweli atawaongoza kwenye ukweli wote; maana hatasema kwa mamlaka yake mwenyewe, bali atawaambieni yote atakayosikia, na atasema mambo yatakayokuwa yanakuja. |
14 |
Yeye atanitukuza mimi kwa kuwa atawaambieni yale atakayopata kutoka kwangu. |
15 |
Vyote alivyo navyo Baba ni vyangu; ndiyo maana nimesema kwamba huyo Roho Mtakatifu atawaambieni yale atakayopata kutoka kwangu. |
16 |
"Bado kitambo kidogo nanyi hamtaniona; na baada ya kitambo kidogo tena mtaniona!" |
17 |
Hapo baadhi ya wanafunzi wake wakaulizana, "Ana maana gani anapotwambia: `Bado kitambo kidogo nanyi hamtaniona; na baada ya kitambo kidogo tena mtaniona?` Tena anasema: `Kwa kuwa ninakwenda kwa Baba!"` |
18 |
Basi, wakawa wanaulizana, "Ana maana gani anaposema: `Bado kitambo kidogo?` Hatuelewi anaongelea nini." |
19 |
Yesu alijua kwamba walitaka kumwuliza, basi akawaambia, "Je, mnaulizana juu ya yale niliyosema: `Bado kitambo kidogo nanyi hamtaniona; na baada ya kitambo kidogo tena mtaniona?` |
20 |
Nawaambieni kweli, ninyi mtalia na kuomboleza, lakini ulimwengu utafurahi: mtaona huzuni lakini huzuni yenu itageuka kuwa furaha. |
21 |
Wakati mama anapojifungua huona huzuni kwa sababu saa ya maumivu imefika; lakini akisha jifungua hayakumbuki tena maumivu hayo kwa sababu ya furaha kwamba mtu amezaliwa duniani. |
22 |
Ninyi pia mna huzuni sasa; lakini nitawajieni tena, nanyi mtajaa furaha mioyoni mwenu, na furaha hiyo hakuna mtu atakayeiondoa kwenu. |
23 |
Siku hiyo hamtaniomba chochote. Kweli nawaambieni, chochote mtakachomwomba Baba kwa jina langu, atawapeni. |
24 |
Mpaka sasa hamjaomba chochote kwa jina langu. Ombeni nanyi mtapata ili furaha yenu ikamilike. |
25 |
"Nimewaambieni mambo hayo kwa mafumbo. Lakini wakati utakuja ambapo sitasema tena nanyi kwa mafumbo, bali nitawaambieni waziwazi juu ya Baba. |
26 |
Siku hiyo mtaomba kwa jina langu, na siwaambii kwamba nitamwomba Baba kwa niaba yenu; |
27 |
maana yeye mwenyewe anawapenda ninyi, kwa sababu ninyi mmenipenda mimi na mmeamini kwamba nimetoka kwa Mungu. |
28 |
Mimi nilitoka kwa Baba, nikaja ulimwenguni; na sasa nauacha ulimwengu na kurudi kwa Baba." |
29 |
Basi, wanafunzi wake wakamwambia, "Ahaa! Sasa unasema waziwazi kabisa bila kutumia mafumbo. |
30 |
Sasa tunajua kwamba wewe unajua kila kitu, na huna haja ya kuulizwa maswali na mtu yeyote; kwa hiyo tunaamini kwamba umetoka kwa Mungu." |
31 |
Yesu akawajibu, "Je, mnaamini sasa? |
32 |
Wakati unakuja, tena umekwisha fika, ambapo ninyi nyote mtatawanyika kila mtu kwake, nami nitaachwa peke yangu. Kumbe, lakini mimi siko peke yangu, maana Baba yu pamoja nami. |
33 |
Nimewaambieni mambo haya ili mpate kuwa na amani katika kuungana nami. Ulimwenguni mtapata masumbuko; lakini jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu!" |