| Chapter 11 |
1 |
Mtu mmoja aitwaye Lazaro, mwenyeji wa Bethania, alikuwa mgonjwa. (Kijiji cha Bethania kilikuwa mahali walipokaa Maria na Martha, dada yake. |
2 |
Maria ndiye yule aliyempaka Bwana marashi na kumpangusa kwa nywele zake. Lazaro, kaka yake, ndiye aliyekuwa mgonjwa.) |
3 |
Basi, hao dada wakatuma ujumbe huu kwa Yesu: "Bwana, rafiki yako ni mgonjwa!" |
4 |
Yesu aliposikia hivyo akasema, "Ugonjwa huo hautaleta kifo, ila ni kwa ajili ya kumtukuza Mungu; ameugua ili kwa njia hiyo Mwana wa Mungu atukuzwe." |
5 |
Yesu aliwapenda Martha, dada yake na Lazaro. |
6 |
Alipopata habari kwamba Lazaro ni mgonjwa, Yesu aliendelea kukaa mahali hapo alipokuwa kwa siku mbili zaidi. |
7 |
Kisha akawaambia wanafunzi wake, "Twendeni tena Yudea!" |
8 |
Wanafunzi wakamwambia, "Mwalimu! Muda mfupi tu umepita tangu Wayahudi walipotaka kukuua kwa mawe, nawe unataka kwenda huko tena?" |
9 |
Yesu akajibu, "Je, saa za mchana si kumi na mbili? Basi, mtu akitembea mchana hawezi kujikwaa kwa kuwa anauona mwanga wa ulimwengu huu. |
10 |
Lakini mtu akitembea usiku atajikwaa kwa maana mwanga haumo ndani yake." |
11 |
Yesu alipomaliza kusema maneno hayo, akawaambia, "Rafiki yetu Lazaro amelala, lakini mimi nitakwenda kumwamsha." |
12 |
Wanafunzi wake wakamwambia, "Bwana, ikiwa amelala, basi atapona." |
13 |
Wao walidhani kwamba alikuwa amesema juu ya kulala usingizi, kumbe alikuwa amesema juu ya kifo cha Lazaro. |
14 |
Basi, Yesu akawaambia waziwazi, "Lazaro amekufa; |
15 |
Lakini nafurahi kwa ajili yenu kwamba sikuwako huko, ili mpate kuamini. Haya, twendeni kwake." |
16 |
Thoma (aitwaye Pacha) akawaambia wanafunzi wenzake, "Twendeni nasi tukafe pamoja naye!" |
17 |
Yesu alipofika huko alikuta Lazaro amekwisha kaa kaburini kwa siku nne. |
18 |
Kijiji cha Bethania kilikuwa karibu na Yerusalemu umbali upatao kilomita tatu. |
19 |
Wayahudi wengi walikuwa wamefika kwa Martha na Maria kuwafariji kwa kifo cha kaka yao. |
20 |
Basi, Martha aliposikia kwamba Yesu alikuwa anakuja, akaenda kumlaki; lakini Maria alibaki nyumbani. |
21 |
Martha akamwambia Yesu, "Bwana, kama ungalikuwa hapa, kaka yangu hangalikufa! |
22 |
Lakini najua kwamba hata sasa chochote utakachomwomba Mungu, atakupa." |
23 |
Yesu akamwambia, "Kaka yako atafufuka." |
24 |
Martha akamjibu, "Najua kwamba atafufuka wakati wa ufufuo, siku ya mwisho." |
25 |
Yesu akamwambia, "Mimi ndimi ufufuo na uzima. Anayeniamini mimi hata kama anakufa, ataishi: |
26 |
na kila anayeishi na kuniamini, hatakufa kamwe. Je, waamini hayo?" |
27 |
Martha akamwambia, "Ndiyo Bwana! Naamini kwamba wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu, yule ajaye ulimwenguni." |
28 |
Baada ya kusema hayo, Martha alikwenda kumwita Maria, dada yake, akamwabia faraghani, "Mwalimu yuko hapa, anakuita." |
29 |
Naye aliposikia hivyo, akainuka mara, akamwendea Yesu. |
30 |
Yesu alikuwa hajaingia kijijini, ila alikuwa bado mahali palepale Martha alipomlaki. |
31 |
Basi, Wayahudi waliokuwa nyumbani pamoja na Maria wakimfariji walipomwona ameinuka na kutoka nje ghafla, walimfuata. Walidhani alikuwa anakwenda kaburini kuomboleza. |
32 |
Basi, Maria alipofika mahali pale Yesu alipokuwa na kumwona, alipiga magoti, akamwabia, "Bwana, kama ungalikuwa hapa, kaka yangu hangalikufa!" |
33 |
Yesu alipomwona analia, na wale Wayahudi waliokuja pamoja naye wanalia pia, alijawa na huzuni na kufadhaika moyoni. |
34 |
Kisha akawauliza, "Mlimweka wapi?" Wakamwambia, "Bwana, njoo uone." |
35 |
Yesu akalia machozi. |
36 |
Basi, Wayahudi wakasema, "Tazameni jinsi alivyompenda!" |
37 |
Lakini baadhi yao wakasema, "Je, huyu aliyemfumbua macho yule kipofu, hakuweza kumfanya Lazaro asife?" |
38 |
Basi, Yesu akiwa amehuzunika tena moyoni, akafika kaburini. Kaburi lenyewe lilikuwa pango, na lilikuwa limefunikwa kwa jiwe. |
39 |
Yesu akasema, "Ondoeni hilo jiwe!" Martha, dada yake huyo aliyekufa, akamwambia, "Bwana, amekwishaanza kunuka; amekaa kaburini siku nne!" |
40 |
Yesu akamwambia, "Je, sikukwambia kwamba ukiamini utaona utukufu wa Mungu?" |
41 |
Basi, wakaliondoa lile jiwe. Yesu akatazama juu mbinguni, akasema, "Nakushukuru Baba kwa kuwa wewe wanisikiliza. |
42 |
Najua kwamba unanisikiliza daima. Lakini nimesema hayo kwa ajili ya watu hawa waliopo hapa ili wapate kuamini kwamba wewe ndiwe uliyenituma." |
43 |
Alipokwisha sema hayo, akaita kwa sauti kubwa: "Lazaro! Toka nje!" |
44 |
Huyo aliyekuwa amekufa akatoka nje, huku amefungwa sanda miguu na mikono, na uso wake umefunikwa. Yesu akawaambia, "Mfungueni, mkamwache aende zake." |
45 |
Basi, Wayahudi wengi waliokuwa wamefika kwa Maria walipoona kitendo hicho alichokifanya Yesu wakamwamini. |
46 |
Lakini baadhi yao walikwenda kwa Mafarisayo wakatoa taarifa ya jambo hilo alilofanya Yesu. |
47 |
kwa hiyo makuhani wakuu na Mafarisayo wakafanya kikao cha Baraza kuu, wakasema, "Tufanye nini? Mtu huyu anafanya ishara nyingi mno. |
48 |
Tukimwacha tu watu wote watamwamini, nao Waroma watakuja kuliharibu Hekalu letu na taifa letu!" |
49 |
Hapo, mmoja wao aitwaye Kayafa, ambaye alikuwa Kuhani Mkuu mwaka huo, akawaambia, "Ninyi hamjui kitu! |
50 |
Je, hamwoni kwamba ni afadhali kwenu mtu mmoja afe kwa ajili ya watu, kuliko taifa zima liangamizwe?" |
51 |
Yeye hakusema hivyo kwa hiari yake mwenyewe, bali kwa vile alikuwa Kuhani Mkuu mwaka huo, alibashiri kwamba Yesu atakufa kwa ajili ya taifa lao; |
52 |
na wala si kwa ajili yao tu, bali pia apate kuwaleta pamoja watoto wa Mungu waliotawanyika. |
53 |
Basi, tangu siku hiyo viongozi wa Wayahudi walifanya mipango ya kumwua Yesu. |
54 |
Kwa hiyo, Yesu hakutembea tena hadharani kati ya Wayahudi, bali alitoka hapo, akaenda mahali karibu na jangwa, katika mji uitwao Efraimu. Akakaa huko pamoja na wanafunzi wake. |
55 |
Sikukuu ya Wayahudi ya Pasaka ilikuwa karibu, na watu wengi walikwenda Yerusalemu ili wajitakase kabla ya sikukuu hiyo. |
56 |
Basi, wakawa wanamtafuta Yesu; nao walipokusanyika pamoja Hekaluni wakaulizana, "Mwaonaje? Yaonekana kwamba haji kabisa kwenye sikukuu, au sivyo?" |
57 |
Makuhani wakuu na Mafarisayo walikuwa wametoa amri kwamba mtu akijua mahali aliko Yesu awaarifu kusudi wamtie nguvuni. |