| Chapter 18 |
1 |
Basi, Yesu aliwasimulia mfano kuonyesha kwamba ni lazima kusali daima bila kukata tamaa. |
2 |
Alisema: "Katika mji mmoja kulikuwa na hakimu ambaye hakuwa anamcha Mungu wala kumjali binadamu. |
3 |
Katika mji huohuo, kulikuwa pia na mama mmoja mjane, ambaye alimwendea huyo hakimu mara nyingi akimwomba amtetee apate haki yake kutoka kwa adui yake. |
4 |
Kwa muda mrefu huyo hakimu hakupenda kumtetea huyo mjane; lakini, mwishowe akajisemea: `Ingawa mimi simchi Mungu wala simjali binadamu, |
5 |
lakini kwa vile huyu mjane ananisumbua, nitamtetea; la sivyo ataendelea kufika hapa, na mwisho atanichosha kabisa!"` |
6 |
Basi, Bwana akaendelea kusema, "Sikieni jinsi alivyosema huyo hakimu mbaya. |
7 |
Je, ndio kusema Mungu hatawatetea wale aliowachagua, ambao wanamlilia mchana na usiku? Je, atakawia kuwasikiliza? |
8 |
Nawaambieni atawatetea upesi. Hata hivyo, je, kutakuwako na imani duniani wakati Mwana wa Mtu atakapokuja?" |
9 |
Halafu Yesu aliwaambia pia mfano wa wale ambao walijiona kuwa wema na kuwadharau wengine. |
10 |
"Watu wawili walipanda kwenda Hekaluni kusali: mmoja Mfarisayo, na mwingine mtoza ushuru. |
11 |
Huyo Mfarisayo akasimama, akasali kimoyomoyo: `Ee Mungu, nakushukuru kwa vile mimi si kama watu wengine: walafi, wadanganyifu au wazinzi. Nakushukuru kwamba mimi si kama huyu mtoza ushuru. |
12 |
Nafunga mara mbili kwa juma, natoa zaka sehemu ya kumi ya pato langu.` |
13 |
Lakini yule mtoza ushuru, akiwa amesimama kwa mbali bila hata kuinua macho yake mbinguni, ila tu akijipiga kifua kwa huzuni, alisema: `Ee Mungu, unionee huruma mimi mwenye dhambi.` |
14 |
Nawaambieni, huyu mtoza ushuru alirudi nyumbani akiwa amesamehewa. Lakini yule mwingine, sivyo. Kwa maana kila anayejikweza atashushwa, na kila anayejishusha atakwezwa." |
15 |
Watu walimletea Yesu watoto wadogo ili awawekee mikono yake. Wanafunzi walipowaona, wakawazuia kwa maneno makali. |
16 |
Lakini Yesu akawaita kwake akisema: "Waacheni hao watoto waje kwangu, wala msiwazuie, kwa maana Ufalme wa Mungu ni kwa ajili ya watu kama hawa. |
17 |
Nawaambieni kweli, mtu yeyote asiyeupokea Ufalme wa Mungu kama mtoto mdogo, hataingia katika Ufalme huo." |
18 |
Kiongozi mmoja, Myahudi, alimwuliza Yesu, "Mwalimu mwema, nifanye nini ili niweze kuupata uzima wa milele?" |
19 |
Yesu akamwambia, "Mbona waniita mwema? Hakuna aliye mwema ila Mungu peke yake. |
20 |
Unazijua amri: `Usizini; usiue; usiibe; usitoe ushahidi wa uongo; waheshimu baba yako na mama yako."` |
21 |
Yeye akasema, "Hayo yote nimeyazingatia tangu ujana wangu." |
22 |
Yesu aliposikia hayo akamwambia, "Unatakiwa bado kufanya kitu kimoja: uza kila ulicho nacho, wagawie maskini, na hivyo utakuwa na hazina yako mbinguni; halafu njoo unifuate." |
23 |
Lakini huyo mtu aliposikia hayo, alihuzunika sana kwa sababu alikuwa tajiri sana. |
24 |
Yesu alipoona akihuzunika hivyo, akasema, "Jinsi gani ilivyo vigumu kwa matajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu! |
25 |
Naam, ni rahisi zaidi kwa ngamia kupita katika tundu la sindano, kuliko tajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu." |
26 |
Wale watu waliposikia hayo, wakasema, "Nani basi, atakayeokolewa?" |
27 |
Yesu akajibu, "Yasiyowezekana kwa binadamu, yanawezekana kwa Mungu." |
28 |
Naye Petro akamwuliza, "Na sisi je? Tumeacha vitu vyote tukakufuata!" |
29 |
Yesu akawaambia, "Kweli nawaambieni, mtu yeyote aliyeacha nyumba au mke au kaka au wazazi au watoto kwa ajili ya Ufalme wa Mungu, |
30 |
atapokea mengi zaidi wakati huu wa sasa, na kupokea uzima wa milele wakati ujao." |
31 |
Yesu aliwachukua kando wale kumi na wawili, akawaambia, "Sikilizeni! Tunakwenda Yerusalemu na huko kila kitu kilichoandikwa na manabii kuhusu Mwana wa Mtu kitakamilishwa. |
32 |
Kwa maana atakabidhiwa kwa watu wa mataifa nao watamtendea vibaya na kumtemea mate. |
33 |
Watampiga mijeledi, watamuua; lakini siku ya tatu atafufuka." |
34 |
Lakini wao hawakuelewa hata kidogo jambo hilo; walikuwa wamefichwa maana ya maneno hayo, na hawakutambua yaliyosemwa. |
35 |
Wakati Yesu alipokaribia Yeriko, kulikuwa na mtu mmoja kipofu ameketi njiani akiomba. |
36 |
Aliposikia umati wa watu ukipita aliuliza, "Kuna nini?" |
37 |
Wakamwambia, "Yesu wa Nazareti anapita." |
38 |
Naye akapaza sauti akisema, "Yesu, Mwana wa Daudi, nihurumie!" |
39 |
Wale watu waliotangulia wakamkemea wakimwambia anyamaze; lakini yeye akazidi kupaza sauti: "Mwana wa Daudi, nihurumie;" |
40 |
Yesu alisimama, akaamuru wamlete mbele yake. Yule kipofu alipofika karibu, Yesu akamwuliza, |
41 |
"Unataka nikufanyie nini?" Naye akamjibu, "Bwana, naomba nipate kuona tena." |
42 |
Yesu akamwambia, "Ona! Imani yako imekuponya." |
43 |
Na mara yule aliyekuwa kipofu akapata kuona, akamfuata Yesu akimtukuza Mungu. Watu wote walipoona hayo, wakamsifu Mungu. |