| Chapter 4 |
1 |
Mafarisayo walisikia kwamba Yesu alikuwa anabatiza na kuwapata wanafunzi wengi kuliko Yohane. |
2 |
Lakini ukweli ni kwamba Yesu hakuwa anabatiza ila wanafunzi wake.) |
3 |
Basi, Yesu aliposikia hayo, alitoka Yudea akarudi Galilaya; |
4 |
na katika safari hiyo ilimbidi apitie Samaria. |
5 |
Basi, akafika Sukari, mji mmoja wa Samaria, karibu na shamba ambalo Yakobo alikuwa amempa mwanawe, Yosefu. |
6 |
Mahali hapo palikuwa na kisima cha Yakobo, naye Yesu, kutokana na uchovu wa safari, akaketi kando ya kisima. Ilikuwa yapata saa sita mchana. |
7 |
Basi, mwanamke mmoja Msamaria akafika kuteka maji. Yesu akamwambia, "Nipatie maji ninywe." |
8 |
(Wakati huo wanafunzi wake walikuwa wamekwenda mjini kununua chakula.) |
9 |
Lakini huyo mwanamke akamwambia, "Wewe ni Myahudi; mimi ni mwanamke Msamaria! Unawezaje kuniomba maji?" (Wayahudi hawakuwa na ushirikiano na Wasamaria katika matumizi ya vitu.) |
10 |
Yesu akamjibu, "Kama tu ungalijua zawadi ya Mungu na ni nani anayekwambia: `Nipatie maji ninywe,` ungalikwisha mwomba, naye angekupa maji yaliyo hai." |
11 |
Huyo mama akasema, "Mheshimiwa, wewe huna chombo cha kutekea maji, nacho kisima ni kirefu; utapata wapi maji yaliyo hai? |
12 |
Au, labda wewe wajifanya mkuu kuliko babu yetu Yakobo? Yeye alitupa sisi kisima hiki; na yeye mwenyewe, watoto wake na mifugo yake walikunywa maji ya kisima hiki." |
13 |
Yesu akamjibu, "Kila anayekunywa maji haya ataona kiu tena. |
14 |
Lakini atakayekunywa maji nitakayompa mimi, hataona kiu milele. Maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji ya uzima na kumpatia uzima wa milele." |
15 |
Huyo mwanamke akamwambia, "Mheshimiwa, nipe maji hayo ili nisione kiu tena; nisije tena mpaka hapa kuteka maji." |
16 |
Yesu akamwambia, "Nenda ukamwite mumeo uje naye hapa." |
17 |
Huyo mwanamke akamwambia, "Mimi sina mume." Yesu akamwambia, "Umesema kweli, kwamba huna mume. |
18 |
Maana umekuwa na waume watano, na huyo unayeishi naye sasa si mume wako. Hapo umesema kweli." |
19 |
Huyo Mwanamke akamwambia, "Mheshimiwa, naona ya kuwa wewe u nabii. |
20 |
Babu zetu waliabudu juu ya mlima huu, lakini ninyi mwasema kwamba mahali pa kumwabudu Mungu ni kule Yerusalemu." |
21 |
Yesu akamwambia, "Niamini; wakati unakuja ambapo hamtamwabudu Baba juu ya mlima huu, wala kule Yerusalemu. |
22 |
Ninyi Wasamaria mnamwabudu yule msiyemjua, lakini sisi tunamjua huyo tunayemwabudu, kwa maana wokovu unatoka kwa Wayahudi. |
23 |
Lakini wakati unakuja, tena umekwisha fika, ambapo wanaoabudu kweli, watamwabudu Baba kwa nguvu ya Roho; watu wanaomwabudu hivyo ndio Baba anaotaka. |
24 |
Mungu ni Roho, na watu wataweza tu kumwabudu kweli kwa nguvu ya Roho wake." |
25 |
Huyo mama akamwambia, "Najua kwamba Masiha, aitwaye Kristo, anakuja. Atakapokuja atatujulisha kila kitu." |
26 |
Yesu akamwambia, "Mimi ninayesema nawe, ndiye." |
27 |
Hapo wanafunzi wake wakarudi, wakastaajabu sana kuona anaongea na mwanamke. Lakini hakuna mtu aliyesema: "Unataka nini?" au, "Kwa nini unaongea na mwanamke?" |
28 |
Huyo mama akauacha mtungi wake pale, akaenda mjini na kuwaambia watu, |
29 |
"Njoni mkamwone mtu aliyeniambia mambo yote niliyotenda! Je, yawezekana kuwa yeye ndiye Kristo?" |
30 |
Watu wakatoka mjini, wakamwendea Yesu. |
31 |
Wakati huohuo wanafunzi wake walikuwa wanamsihi Yesu: "Mwalimu, ule chakula." |
32 |
Lakini Yesu akawaambia, "Mimi ninacho chakula msichokijua ninyi." |
33 |
Wanafunzi wake wakaulizana, "Je, kuna mtu aliyemletea chakula?" |
34 |
Yesu akawaambia, "Chakula changu ni kufanya anachotaka yule aliyenituma na kuitimiza kazi yake. |
35 |
Ninyi mwasema: `Bado miezi minne tu, na wakati wa mavuno utafika!` Lakini mimi nawaambieni, yatazameni mashamba; mazao yako tayari kuvunwa. |
36 |
Mvunaji anapata mshahara wake, na anakusanya mavuno kwa ajili ya uzima wa milele; hivyo mpandaji na mvunaji watafurahi pamoja. |
37 |
Kwa sababu hiyo msemo huu ni kweli: `Mmoja hupanda na mwingine huvuna.` |
38 |
Mimi nimewatuma mkavune mavuno ambayo hamkuyatolea jasho, wengine walifanya kazi, lakini ninyi mnafaidika kutokana na jasho lao." |
39 |
Wasamaria wengi wa kijiji kile waliamini kwa sababu ya maneno aliyosema huyo mama: "Ameniambia mambo yote niliyofanya." |
40 |
Wasamaria walimwendea Yesu wakamwomba akae nao; naye akakaa hapo siku mbili. |
41 |
Watu wengi zaidi walimwamini kwa sababu ya ujumbe wake. |
42 |
Wakamwambia yule mama, "Sisi hatuamini tu kwa sababu ya maneno yako; sisi wenyewe tumesikia, na tunajua kwamba huyu ndiye kweli Mwokozi wa ulimwengu." |
43 |
Baada ya siku mbili Yesu aliondoka hapo, akaenda Galilaya. |
44 |
Maana Yesu mwenyewe alisema waziwazi kwamba, "Nabii hapati heshima katika nchi yake." |
45 |
Basi, alipofika Galilaya, Wagalilaya wengi walimkaribisha. Maana nao pia walikuwa kwenye sikukuu ya Pasaka, wakayaona mambo yote Yesu aliyotenda huko Yerusalemu wakati wa sikukuu hiyo. |
46 |
Yesu alifika tena huko mjini Kana, mkoani Galilaya, mahali alipogeuza maji kuwa divai. Kulikuwa na ofisa mmoja aliyekuwa na mtoto mgonjwa huko Kafarnaumu. |
47 |
Basi, huyo ofisa aliposikia kuwa Yesu alikuwa ametoka Yudea na kufika Galilaya, alimwendea akamwomba aende kumponya mtoto wake aliyekuwa mgonjwa mahututi. |
48 |
Yesu akamwambia, "Msipoona ishara na maajabu hamtaamini!" |
49 |
Huyo ofisa akamwambia, "Mheshimiwa, tafadhali twende kabla mwanangu hajafa." |
50 |
Yesu akamwambia, "Nenda tu, mwanao yu mzima." Huyo mtu akaamini maneno ya Yesu, akaenda zake. |
51 |
Alipokuwa bado njiani, watumishi wake walikutana naye, wakamwambia kwamba mwanawe alikuwa mzima. |
52 |
Naye akawauliza saa mtoto alipopata nafuu; nao wakamwambia, "Jana saa saba mchana, homa ilimwacha." |
53 |
Huyo baba akakumbuka kwamba ilikuwa ni saa ileile ambapo Yesu alimwambia: "Mwanao yu mzima." Basi, yeye akaamini pamoja na jamaa yake yote. |
54 |
Hii ilikuwa ishara ya pili aliyoifanya Yesu alipokuwa anatoka Yudea kwenda Galilaya. |