| Chapter 3 |
1 |
Yesu aliingia tena katika sunagogi na mle ndani mlikuwa na mtu aliyekuwa na mkono uliopooza. |
2 |
Humo baadhi ya watu walimngojea amponye mtu huyo siku ya sabato ili wapate kumshtaki. |
3 |
Yesu akamwambia huyo mtu aliyekuwa na mkono uliopooza, "Njoo hapa katikati." |
4 |
Kisha, akawauliza, "Je, ni halali siku ya Sabato kutenda jambo jema au kutenda jambo baya; kuokoa maisha au kuua?" Lakini wao hawakusema neno. |
5 |
Hapo akawatazama wote kwa hasira, akaona huzuni kwa sababu ya ugumu wa mioyo yao. Kisha akamwambia huyo mtu, "Nyosha mkono wako!" Naye akaunyosha mkono wake, ukawa mzima tena. |
6 |
Mara Mafarisayo wakatoka nje, wakafanya shauri pamoja na watu wa kikundi cha Herode jinsi ya kumwangamiza Yesu. |
7 |
Yesu aliondoka hapo pamoja na wanafunzi wake, akaenda kando ya ziwa, na umati wa watu ukamfuata. Watu hao walikuwa wametoka Yerusalemu, Yudea, |
8 |
Idumea, ng`ambo ya mto Yordani, Tiro na Sidoni. Watu hao wengi walimwendea Yesu kwa sababu ya kusikia mambo mengi aliyokuwa ameyatenda. |
9 |
Yesu akawaambia wanafunzi wake wamtayarishie mashua moja, ili umati wa watu usije ukamsonga. |
10 |
Alikuwa amewaponya watu wengi, na wagonjwa wote wakawa wanamsonga ili wapate kumgusa. |
11 |
Na watu waliokuwa wamepagawa na pepo wachafu walipomwona, walijitupa chini mbele yake na kupaaza sauti, "Wewe ni Mwana wa Mungu!" |
12 |
Lakini Yesu akawaamuru kwa ukali wasimjulishe kwa watu. |
13 |
Yesu alipanda kilimani, akawaita wale aliowataka. Basi, wakamwendea, |
14 |
naye akawateua watu kumi na wawili ambao aliwaita mitume,*fb* wakae naye, awatume kuhubiri |
15 |
na wawe na mamlaka ya kuwafukuza pepo. |
16 |
Basi, hao kumi na wawili walioteuliwa ndio hawa: Simoni (ambaye Yesu alimpa jina, Petro), |
17 |
Yakobo na Yohane, wana wa Zebedayo (Yesu aliwapa hawa ndugu wawili jina Boanerge, maana yake "wanangurumo"), |
18 |
Andrea na Filipo, Batholomayo, Mathayo, Thoma, Yakobo mwana wa Alfayo, Thadayo, Simoni Mkanani na |
19 |
Yuda Iskarioti ambaye alimsaliti Yesu. |
20 |
Kisha Yesu alikwenda nyumbani. Umati wa watu ukakusanyika tena, hata Yesu na wafuasi wake wasiweze kupata nafasi ya kula chakula. |
21 |
Basi, watu wa jamaa yake walipopata habari hiyo wakatoka kwenda kumchukua maana walikuwa wanasema kwamba amepatwa na wazimu. |
22 |
Nao walimu wa Sheria waliokuwa wametoka Yerusalemu, wakasema, "Ana Beelzebuli! Tena, anawafukuza pepo kwa nguvu ya mkuu wa pepo." |
23 |
Hapo Yesu akawaita, akawaambia kwa mifano,"Shetani anawezaje kumfukuza Shetani? |
24 |
Ikiwa utawala mmoja umegawanyika makundimakundi yanayopigana, utawala huo hauwezi kudumu. |
25 |
Tena, ikiwa jamaa moja imegawanyika makundimakundi yanayopingana, jamaa hiyo itaangamia. |
26 |
Ikiwa basi, utawala wa Shetani umegawanyika vikundivikundi hauwezi kudumu, bali utaangamia kabisa. |
27 |
"Hakuna mtu awezaye kuivamia nyumba ya mtu mwenye nguvu na kumnyang`anya mali yake, isipokuwa kwanza amemfunga huyo mtu mwenye nguvu; hapo ndipo atakapoweza kumnyang`anya mali yake. |
28 |
"Kweli nawaambieni, watu watasamehewa dhambi zao zote na kufuru zao zote; |
29 |
lakini anayesema mabaya dhidi ya Roho Mtakatifu, hatasamehewa kamwe; ana hatia ya dhambi ya milele." |
30 |
Yesu alisema hivyo kwa sababu walikuwa wanasema, "Ana pepo mchafu.") |
31 |
Mama yake Yesu na ndugu zake walifika hapo, wakasimama nje, wakampelekea ujumbe kutaka kumwona. |
32 |
Umati wa watu ulikuwa umekaa hapo kumzunguka. Basi, wakamwambia, "Mama yako na ndugu zako wako nje, wanataka kukuona." |
33 |
Yesu akawaambia, "Mama yangu na ndugu zangu ni kina nani?" |
34 |
Hapo akawatazama watu waliokuwa wamemzunguka, akasema, "Tazameni! Hawa ndio mama yangu na ndugu zangu. |
35 |
Mtu yeyote anayefanya anayotaka Mungu, huyo ndiye kaka yangu, dada yangu na mama yangu." |