| Chapter 5 |
1 |
Kristo alitupa uhuru akataka tubaki huru. Basi, simameni imara wala msikubali tena kuwa chini ya nira ya utumwa. |
2 |
Sikilizeni! Ni mimi Paulo ninayesema nanyi! Kama mkikubali kutahiriwa, Kristo hatawafaidia chochote. |
3 |
Nasema tena wazi: kila anayekubali kutahiriwa itambidi kuishika Sheria yote. |
4 |
Kama mnatazamia kukubaliwa kuwa waadilifu kwa njia ya Sheria, basi, mmejitenga mbali na Kristo; mko nje ya neema ya Mungu. |
5 |
Kwa upande wetu, lakini, sisi tunatumaini kwamba kwa nguvu ya Roho tunakubaliwa kuwa waadilifu kwa njia ya imani. |
6 |
Maana ikiwa tumeungana na Kristo Yesu, kutahiriwa au kutotahiriwa hakuna maana; cha maana ni imani ifanyayo kazi kwa mapendo. ic |
7 |
Mwenendo wenu ulikuwa mzuri! Nani, basi aliyewazuia kuuzingatia ukweli? |
8 |
Aliyesababisha hali hiyo si Mungu ambaye amewaiteni. |
9 |
"chachu kidogo tu huchachusha donge lote la unga!" |
10 |
Kutokana na kuungana kwetu na Bwana, nina tumaini kubwa kwamba ninyi hamtakuwa na msimamo tofauti nami. Tena yeyote huyo anayewavurugeni--awe nani au nani--hakika ataadhibiwa. |
11 |
Na kwa upande wangu, ndugu zangu, kama bado ninahubiri kwamba kutahiriwa ni lazima, kwa nini basi, bado ninadhulumiwa? Kama ingalikuwa hivyo, mahubiri yangu juu ya msalaba wa Kristo yasingalileta aibu yoyote. |
12 |
Laiti hao wanaowavurugeni wangejikatakata wenyewe! |
13 |
Ninyi, ndugu, mliitwa muwe watu huru. Lakini uhuru huo usiwe kisingizio cha kutawaliwa na tamaa za kidunia; ila mnapaswa kutumikiana kwa upendo. |
14 |
Maana Sheria yote hutimizwa katika kushika amri hii moja: "Mpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe." |
15 |
Lakini ikiwa mtaumana na kutafunana kama wanyama, jihadharini msije mkaangamizana wenyewe kwa wenyewe! |
16 |
Basi, nasema hivi: mwenendo wenu na uongozwe na Roho, nanyi hamtafuata tena tamaa za kidunia. |
17 |
Maana, tamaa za kidunia hupingana na matakwa ya Roho; na matakwa ya Roho hupingana na tamaa za kidunia. Mambo hayo mawili hayaafikiani; kwa sababu hiyo hamwezi kufanya yale mnayotaka ninyi wenyewe. |
18 |
Kama mkiongozwa na Roho, basi, hamko tena chini ya Sheria. |
19 |
Basi, matendo ya kidunia yanajulikana: uzinzi, uasherati, ufisadi; |
20 |
kuabudu sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, choyo, mabishano, mafarakano; |
21 |
husuda, ulevi, ulafi na mambo mengine kama hayo. Nawaambieni tena kama nilivyokwisha sema: watu wanaotenda mambo hayo hawatakuwa na nafasi yao katika ufalme wa Mungu. |
22 |
Lakini matokeo ya kuongozwa na Roho ni mapendo, furaha, amani, uvumilivu, wema, fadhili, uaminifu, |
23 |
upole na kuwa na kiasi. Hakuna Sheria inayoweza kupinga mambo hayo. |
24 |
Wale walio wa Kristo wameisulubisha hali yao ya kidunia pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake. |
25 |
Tukiishi kwa msaada wa Roho, na tuufuate mwongozo wake. |
26 |
Basi, tusijivune, tusichokozane wala kuoneana wivu. |